Afya; Madhara Ya Nguo Za Kubana Yanawasumbua Wengi

 post-feature-image
Siku hizi kuna mtindo wa watu wengi, hasa vijana, kuvaa mavazi yanayowabana. Wao wanadai ndiyo mitindo ya kisasa ambayo mtu akiifuata anakuwa anaenda na wakati.

Wengi huona kuwa kuvaa vile ni kwenda na wakati. Kutokana na hali hii, ni jambo gumu kutenganisha mitindo ya mavazi na mfumo wa kila siku wa maisha ya binadamu. Kila siku watengenezaji wa nguo na wabunifu wa mitindo ya mavazi kwa kushirikiana na wafanyabiashara, wanabuni mitindo mipya na kuiingiza sokoni kwa kuitangaza na kuipamba ili kupata mauzo mazuri.
Uchunguzi unaonyesha kuwa biashara ya nguo zinazobana mwili ndizo zinazofanya vizuri kwenye soko. Watu wengi hasa vijana wanapenda mitindo mipya kama njia ya kuwafanya waonekane watu nadhifu, watanashati, wenye uwezo wa kifedha, watu wanaokwenda na wakati na wenye mvuto wa maumbile ya mwili.
Baadhi ya watu wachache wanaovaa nguo za kubana wanafanya hivyo huku wakiwa wanafahamu madhara yake, lakini walio wengi hawana habari kuhusu matatizo ya kiafya yanayoweza kuwapata.
Madaktari wengi wamekuwa wakiwaonya watu kuhusu hatari za kiafya zinazotokana na kuvaa kwa muda mrefu nguo zinazobana sana kwa lengo la kutengeneza umbo la mwili linalovutia. “Sote tunapenda njia za mkato zisizohitaji kufanya jitihada, lakini njia hizi zina madhara na hazitusaidii kama ambavyo tungepata faida kwa kufanya mazoezi na kutumia lishe nzuri,” anasema Orly Avitzur, daktari bingwa wa mfumo wa fahamu nchini Marekani.
Mbali na ukweli kwamba baadhi ya mitindo ya mavazi inasababisha adha kubwa kwa watumiaji, mitindo mingine husababisha athari mbaya kwa afya kwa watumiaji na jamii kwa ujumla.
Miongoni mwa mitindo ya mavazi inayosababisha athari mbaya za kiafya ni ile ya mavazi yanayobana sana. Tafiti kadhaa za kisayansi zinabainisha kuwa miongoni mwa nguo zinazoathiri afya ni nguo za ndani za wanaume zinazobana sana maarufu kama kama boksa pamoja na suruali za jeans zinazobana maarufu kama ‘skinny jeans’ ambazo mara nyingi huvaliwa na wanawake.
Nguo zinazobana sana husababisha mishipa midogomidogo inayosafirisha damu kubanwa na kuathiri usambazaji wa damu kwenye baadhi ya maeneo ya mwili.
Kutokana na hali ya kubana, nguo hizo husababisha uharibifu wa misuli na mishipa ya fahamu katika mapaja na miguu hasa kwa wanawake. Mara nyingi madhara ya nguo hizi hujitokeza kama dalili ya miguu kufa ganzi au hisia za miguu kuwaka moto na ni mara chache wahusika kutambua kuwa dalili hizo chanzo chake ni mavazi.
Katika ripoti ya hivi karibuni iliyochapishwa Juni mwaka 23, mwaka jana na Jarida la Neurology, Neurosurgery and Psychiatry, inaonyesha kuwa watafiti katika Hospitali ya Royal Adelaide nchini Australia walihusisha nguo za kubana sana za aina ya jeans na kutokea kwa tatizo la misuli lijulikanalo kitabibu kama compartiment syndrome ambalo alilipata mwanamke mmoja nchini humo.
“Ugonjwa wa mwanamke huyu unaonyesha madhara mapya ya uvaaji wa jeans zinazobana.” alisema Dk Thomas Kimber, mmoja wa watafiti waliotoa ripoti hiyo alipokuwa akizungumza kuhusu madhara ya mavazi ya kubana.
Mtaalamu wa mishipa ya fahamu na mwanachama wa chama cha Madaktari wa Mishipa ya Fahamu cha Marekani (AAM), Dk John England, anasema: “Mishipa ya fahamu kwa baadhi ya watu, inaweza kukandamizwa kwa urahisi. Mshipa wa femoral cutaneous unaotoka kwenye nyonga na kuingia mapajani kwa ajili ya kuchukua hisia, unaweza kubanwa na kitu chochote kinachobana mapaja au eneo la kiuno.” Hali ya kubanwa kwa mishipa ya fahamu kama itakuwa ya kujirudia rudia inaweza kusababisha madhara ya kudumu.

Madhara ya nguo za kubana

Kwa wanawake nguo zinazobana kupita kiasi zinaweza kusababisha damu kuganda ndani ya mishipa, uvimbe wa mishipa ya damu kwenye miguu na magonjwa ya fangasi ya ngozi yanayoambatana na muwasho.
Hii inaweza kutokea kwa sababu ya jasho linalozalisha kwa wingi katika nguo zinazobana na kufanya ngozi ikose hewa safi.
Uvimbe wa mishipa ya damu miguuni maarufu kama vericose veins, ni moja ya matatizo yanayowapata mara kwa mara wanawake wajawazito na wale wanaotumia vidonge, vipandikizi na sindano za kupanga uzazi bila kufanya mazoezi ya mwili.
Tatizo jingine kwa mujibu wa utafiti uliochapishwa mwaka 2004 katika toleo namba 117(2) la Jarida la Ejog (Europian Journal of Obstetrics & Gynaecology and Reproductive Biology) ni ongezeko la kuzaliana kwa bakteria waharibifu ambao wanasababisha mwanamke kutokwa na usaha katika sehemu za siri.
Hali inaweza kuwa mbaya zaidi kwa wanawake wanene na watu wenye tatizo la ugonjwa wa kisukari.
Kwa wanaume, mavazi haya yanaweza kuathiri utendaji wa figo pamoja na kibofu cha mkojo na kuchochea kutokea kwa maambukizi katika njia ya mfumo wa mkojo.
Yanaweza pia kusababisha uvimbe wa mishipa ya korodani au makende na kuathiri ubora wa mbegu za kiume. Hali hii wakati mwingine huwa ni chanzo cha ugumba na upungufu wa nguvu za kiume kutokana na athari za maumbile ya kianatomi pamoja na athari za kisaikolojia.
Utafiti ulioongozwa na Dk F. Parazzini wa nchini Italy na kuchapishwa mwaka 1995 katika Jarida la International of andrology toleo namba 18(3), ulionyesha kuwa, uvaaji wa nguo zinazobana unaathiri uwezo wa wanaume kuzalisha mbegu za kutosha.
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Wanawake na Uzazi katika Hosipitali ya Taifa Muhimbili, Dk Cyril Massawe anasema athari za mavazi haya yapo mengi na mbaya zaidi ni yale yanayogandamiza mfumo wa uzazi wa mwanaume. Anaonya kwamba watu wengi wanaovutiwa na mavazi hayo hasa vijana, wanapaswa kuwa makini kwa sababu tafiti zilizofadhwa zimethibitisha watu kuathirika.
“Mwanaume ili kuhifadhi vizuri mbegu zake, anatakiwa kutumia mavazi yenye kupitisha hewa,” anasema Dk Massawe.
Kutokana na athari za muda mfupi na zile za muda mrefu za mavazi yanayobana sana mwili, mtaalamu huyo wa afya anaonya jamii haina budi kuzingatia afya na usalama kwanza kabla ya kufikiria urembo na kupendeza.
“Ni muhimu kukumbuka kuwa urembo na utanashati bila afya njema ni sawa na kujificha katika kichaka cha karanga,” anaonya kwa usemi huo wa Kiswahili. Karanga ni mmea unaoota kwa mfano wa kichaka lakini urefu wake hauzidi sentimita 20 hivyo hauwezi kumsitiri mtu, ili ajifiche, asionekane.

Je, tabia hii yaweza kukoma?

Ni vigumu kubadili mitindo ya mavazi ambayo inashabikiwa hasa ikizingatiwa kuwa athari zake si za wazi. Mtu anaweza kusema kuwa amevaa mavazi ya namna hiyo kwa muda mrefu lakini hajaona madhara. Lakini ukweli ni kwamba athari zake zinaweza zisionekane wazi lakini zikawa ni za polepole na ambazo zitasababisha madhara makubwa miaka ijayo.
Suala la kubadili tabia ni la mtu binafsi na ni jambo ambalo litatokana na mhusika baada ya kupima faida na madhara ya mavazi haya yanayopendwa zaidi.
Ni suala la mtu kujiuliza; nionekane mtu wa kisasa kwa wakati huu mbele za watu na baadaye niwe na matatizo ya kiafya au niachane na mambo ya kuiga ili niwe na afya njema maishani.
Kuonekana nadhifu na mtanashati siyo lazima kuvaa mavazi yanayobana sana. Waweza kuvaa mavazi yanayoruhusu mwili kutoathirika na ukaonekana nadhifu.
Tatizo hapa ni ile hali ya kuvaa mavazi yanayobana mwili na wengine ingawa wanajihisi vibaya huvumilia. Kumbuka kuwa na afya bora kwa sasa na siku za baadaye za maisha yako ni jambo muhimu katika kukufanya uishi miaka mingi duniani.
Source; www.tubongetz.com
Share on Google Plus

About Unknown

0 comments:

Post a Comment