
Siku hizi kuna mtindo wa watu wengi, hasa vijana, kuvaa mavazi
yanayowabana. Wao wanadai ndiyo mitindo ya kisasa ambayo mtu akiifuata
anakuwa anaenda na wakati.
Wengi huona kuwa kuvaa vile ni kwenda na wakati. Kutokana na hali hii,
ni jambo gumu kutenganisha mitindo ya mavazi na mfumo wa kila siku wa
maisha ya binadamu. Kila siku watengenezaji wa nguo na wabunifu wa
mitindo ya mavazi kwa kushirikiana na wafanyabiashara, wanabuni mitindo
mipya na kuiingiza sokoni kwa kuitangaza na kuipamba ili kupata mauzo
mazuri.
Uchunguzi unaonyesha kuwa biashara ya nguo zinazobana mwili ndizo
zinazofanya vizuri kwenye soko. Watu wengi hasa vijana wanapenda mitindo
mipya kama njia ya kuwafanya waonekane watu nadhifu, watanashati, wenye
uwezo wa kifedha, watu wanaokwenda na wakati na wenye mvuto wa maumbile
ya mwili.
Baadhi ya watu wachache wanaovaa nguo za kubana wanafanya hivyo huku
wakiwa wanafahamu madhara yake, lakini walio wengi hawana habari kuhusu
matatizo ya kiafya yanayoweza kuwapata.
Madaktari wengi wamekuwa wakiwaonya watu kuhusu hatari za kiafya
zinazotokana na kuvaa kwa muda mrefu nguo zinazobana sana kwa lengo la
kutengeneza umbo la mwili linalovutia. “Sote tunapenda njia za mkato
zisizohitaji kufanya jitihada, lakini njia hizi zina madhara na
hazitusaidii kama ambavyo tungepata faida kwa kufanya mazoezi na kutumia
lishe nzuri,” anasema Orly Avitzur, daktari bingwa wa mfumo wa fahamu
nchini Marekani.
Mbali na ukweli kwamba baadhi ya mitindo ya mavazi inasababisha adha
kubwa kwa watumiaji, mitindo mingine husababisha athari mbaya kwa afya
kwa watumiaji na jamii kwa ujumla.
Miongoni mwa mitindo ya mavazi inayosababisha athari mbaya za kiafya ni
ile ya mavazi yanayobana sana. Tafiti kadhaa za kisayansi zinabainisha
kuwa miongoni mwa nguo zinazoathiri afya ni nguo za ndani za wanaume
zinazobana sana maarufu kama kama boksa pamoja na suruali za jeans
zinazobana maarufu kama ‘skinny jeans’ ambazo mara nyingi huvaliwa na
wanawake.
Nguo zinazobana sana husababisha mishipa midogomidogo inayosafirisha
damu kubanwa na kuathiri usambazaji wa damu kwenye baadhi ya maeneo ya
mwili.
Kutokana na hali ya kubana, nguo hizo husababisha uharibifu wa misuli na
mishipa ya fahamu katika mapaja na miguu hasa kwa wanawake. Mara nyingi
madhara ya nguo hizi hujitokeza kama dalili ya miguu kufa ganzi au
hisia za miguu kuwaka moto na ni mara chache wahusika kutambua kuwa
dalili hizo chanzo chake ni mavazi.
Katika ripoti ya hivi karibuni iliyochapishwa Juni mwaka 23, mwaka jana
na Jarida la Neurology, Neurosurgery and Psychiatry, inaonyesha kuwa
watafiti katika Hospitali ya Royal Adelaide nchini Australia walihusisha
nguo za kubana sana za aina ya jeans na kutokea kwa tatizo la misuli
lijulikanalo kitabibu kama compartiment syndrome ambalo alilipata mwanamke mmoja nchini humo.
“Ugonjwa wa mwanamke huyu unaonyesha madhara mapya ya uvaaji wa jeans
zinazobana.” alisema Dk Thomas Kimber, mmoja wa watafiti waliotoa
ripoti hiyo alipokuwa akizungumza kuhusu madhara ya mavazi ya kubana.
Mtaalamu wa mishipa ya fahamu na mwanachama wa chama cha Madaktari wa
Mishipa ya Fahamu cha Marekani (AAM), Dk John England, anasema:
“Mishipa ya fahamu kwa baadhi ya watu, inaweza kukandamizwa kwa urahisi.
Mshipa wa femoral cutaneous unaotoka kwenye nyonga na kuingia
mapajani kwa ajili ya kuchukua hisia, unaweza kubanwa na kitu chochote
kinachobana mapaja au eneo la kiuno.” Hali ya kubanwa kwa mishipa ya
fahamu kama itakuwa ya kujirudia rudia inaweza kusababisha madhara ya
kudumu.
Madhara ya nguo za kubana
Kwa wanawake nguo zinazobana kupita kiasi zinaweza kusababisha damu
kuganda ndani ya mishipa, uvimbe wa mishipa ya damu kwenye miguu na
magonjwa ya fangasi ya ngozi yanayoambatana na muwasho.
Hii inaweza kutokea kwa sababu ya jasho linalozalisha kwa wingi katika nguo zinazobana na kufanya ngozi ikose hewa safi.
Uvimbe wa mishipa ya damu miguuni maarufu kama vericose veins, ni moja
ya matatizo yanayowapata mara kwa mara wanawake wajawazito na wale
wanaotumia vidonge, vipandikizi na sindano za kupanga uzazi bila kufanya
mazoezi ya mwili.
Tatizo jingine kwa mujibu wa utafiti uliochapishwa mwaka 2004 katika
toleo namba 117(2) la Jarida la Ejog (Europian Journal of Obstetrics
& Gynaecology and Reproductive Biology) ni ongezeko la kuzaliana kwa
bakteria waharibifu ambao wanasababisha mwanamke kutokwa na usaha
katika sehemu za siri.
Hali inaweza kuwa mbaya zaidi kwa wanawake wanene na watu wenye tatizo la ugonjwa wa kisukari.
Kwa wanaume, mavazi haya yanaweza kuathiri utendaji wa figo pamoja na
kibofu cha mkojo na kuchochea kutokea kwa maambukizi katika njia ya
mfumo wa mkojo.
Yanaweza pia kusababisha uvimbe wa mishipa ya korodani au makende na
kuathiri ubora wa mbegu za kiume. Hali hii wakati mwingine huwa ni
chanzo cha ugumba na upungufu wa nguvu za kiume kutokana na athari za
maumbile ya kianatomi pamoja na athari za kisaikolojia.
Utafiti ulioongozwa na Dk F. Parazzini wa nchini Italy na kuchapishwa
mwaka 1995 katika Jarida la International of andrology toleo namba
18(3), ulionyesha kuwa, uvaaji wa nguo zinazobana unaathiri uwezo wa
wanaume kuzalisha mbegu za kutosha.
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Wanawake na Uzazi katika Hosipitali ya
Taifa Muhimbili, Dk Cyril Massawe anasema athari za mavazi haya yapo
mengi na mbaya zaidi ni yale yanayogandamiza mfumo wa uzazi wa mwanaume.
Anaonya kwamba watu wengi wanaovutiwa na mavazi hayo hasa vijana,
wanapaswa kuwa makini kwa sababu tafiti zilizofadhwa zimethibitisha watu
kuathirika.
“Mwanaume ili kuhifadhi vizuri mbegu zake, anatakiwa kutumia mavazi yenye kupitisha hewa,” anasema Dk Massawe.
Kutokana na athari za muda mfupi na zile za muda mrefu za mavazi
yanayobana sana mwili, mtaalamu huyo wa afya anaonya jamii haina budi
kuzingatia afya na usalama kwanza kabla ya kufikiria urembo na
kupendeza.
“Ni muhimu kukumbuka kuwa urembo na utanashati bila afya njema ni sawa
na kujificha katika kichaka cha karanga,” anaonya kwa usemi huo wa
Kiswahili. Karanga ni mmea unaoota kwa mfano wa kichaka lakini urefu
wake hauzidi sentimita 20 hivyo hauwezi kumsitiri mtu, ili ajifiche,
asionekane.
Je, tabia hii yaweza kukoma?
Ni vigumu kubadili mitindo ya mavazi ambayo inashabikiwa hasa
ikizingatiwa kuwa athari zake si za wazi. Mtu anaweza kusema kuwa amevaa
mavazi ya namna hiyo kwa muda mrefu lakini hajaona madhara. Lakini
ukweli ni kwamba athari zake zinaweza zisionekane wazi lakini zikawa ni
za polepole na ambazo zitasababisha madhara makubwa miaka ijayo.
Suala la kubadili tabia ni la mtu binafsi na ni jambo ambalo litatokana
na mhusika baada ya kupima faida na madhara ya mavazi haya yanayopendwa
zaidi.
Ni suala la mtu kujiuliza; nionekane mtu wa kisasa kwa wakati huu mbele
za watu na baadaye niwe na matatizo ya kiafya au niachane na mambo ya
kuiga ili niwe na afya njema maishani.
Kuonekana nadhifu na mtanashati siyo lazima kuvaa mavazi yanayobana
sana. Waweza kuvaa mavazi yanayoruhusu mwili kutoathirika na ukaonekana
nadhifu.
Tatizo hapa ni ile hali ya kuvaa mavazi yanayobana mwili na wengine
ingawa wanajihisi vibaya huvumilia. Kumbuka kuwa na afya bora kwa sasa
na siku za baadaye za maisha yako ni jambo muhimu katika kukufanya uishi
miaka mingi duniani.
Source; www.tubongetz.com
Source; www.tubongetz.com
0 comments:
Post a Comment